Tanzania inaendelea kunufaika na miradi mikubwa ya mikopo yenye masharti nafuu inayotolewa kupitia Benki ya Exim ya China ikiwa ni pamoja na Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme ya Kilovolti (kV) 400 Kaskazini-Mashariki (Dar es Salaam–Arusha) na mradi Upanuzi wa Mawasiliano ya Mtandao wa Simu Vijijini (Awamu ya Kwanza).

Hayo yamebainishwa jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Ali Munde (Mb) wakati wa mkutano na ujumbe wa Benki ya Exim ya China ulioongozwa na Naibu Meneja Mkuu wa Benki hiyo, Bi. Liu Fang.

Mhe. Munde alisema kuwa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme Dar es Salaam–Arusha na Uboreshaji wa Mfumo wa umeme Awamu ya Kwanza una thamani ya Dola za Marekani milioni 270.3 na Mradi wa Upanuzi wa Mawasiliano ya Mtandao wa Simu Vijijini Awamu ya Kwanza una thamani ya Dola za Marekani milioni 108.6.

“Miradi hii miwili inayoendelea yenye jumla ya thamani ya Dola za Marekani milioni 378.9, ambayo mikataba yake ilisainiwa tarehe 27 Septemba 2025, ni muhimu katika kuboresha uhakika wa upatikanaji wa umeme katika Gridi ya Taifa na kukuza ujumuishaji wa kidijitali katika maeneo ya vijijini”, alisema Mhe. Munde.

Vile vile Mhe. Munde alisema kuwa Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Benki ya Exim ya China kwa sasa iko katika hatua za mwisho za majadiliano kuhusu Rasimu ya Mkataba wa Mkopo wa masharti nafuu kwa ajili ya kugharamia Mradi wa Uanzishaji wa Vyuo vinne vya Ufundi Stadi (TVET) katika maeneo ya Zanzibar, Kigoma, Mtwara na Mwanza (Awamu ya Kwanza).

Alisema kuwa Mpango huo unatarajiwa kuongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wa elimu ya ufundi na mafunzo ya stadi za kazi nchini na hivyo kuchangia katika maendeleo ya ujuzi na ajira kwa vijana.

Pia ameitaka Benki ya Exim ya China kuangalia namna ya kusaidia upatikanaji wa fedha kwa ajili ya mradi wa Umeme wa kV 400 Chalinze Segera, kV 220 Segera Tanga na njia ya umeme ya Chalinze – Bagamoyo na vituo vyake na Mtandao wa Mawasiliano Vijijini Awamu ya Pili.

Aidha Mhe. Munde alifikisha salamu na shukrani kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akieleza kuthamini ushirikiano wa muda mrefu uliopo kati ya Tanzania na China.

Alitoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa kuendelea kutoa msaada unaoendana kwa karibu na vipaumbele vya maendeleo ya Taifa vilivyoainishwa katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (2021/22–2025/26) pamoja na Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2025.

Kwa upande wake Kiongozi wa ujumbe wa Benki ya Exim ya China na Naibu Meneja Mkuu, wa Benki hiyo Bi. Liu Fang alisema kuwa Benki yake itaendelea kushirikiana na Tanzania katika maeneo ya vipaumbele vitakavyowezesha kuchochea maendeleo na kutimiza malengo ya Dira 2050.

Aliyataja baadhi ya maeneo yatakayozingatiwa kuwa ni pamoja na miradi ya Nishati, Miundombinu ya Usafirishaji, TEHAMA na mengine ambayo itaongeza wigo wa maendeleo na kuimarisha ushirikiano kati ya pande hizo mbili.

Bi. Fang ameipongeza Tanzania kwa kupiga hatua kubwa katika maendeleo ya uchumi kwa kuwa si tu amesoma katika taarifa mbalimbali lakini pia ameshuhudia kaika ziara yake inayoendelea nchini Tanzania.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *