Na Mwandishi Wetu
Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu Huruia Tanzania (OUT), Dk Yohana Lawi amesema uwekezaji katika sekta ya gesi ni suala la kisera.
“Kama Taifa na Serikali, sera yetu katika matumizi ya gesi asilia inatoa kipaumbele kiasi gani na maelekezo gani kwenye matumizi ya gesi asilia, suala la kupata wawekezaji na kupata vituo ni jambo dogo kwa sababu ili wafungue vituo wanahitaji wateja lakini tuna sera gani?” amehoji.
Amesema endapo kuna sera inayoelekeza magari na mitambo viwandani kufikia miaka ijayo ziwe zinatumia gesi asilia kungesaidia kuvutia wawekezaji katika nishati hiyo.
Dk Lawi ametoa mfano wa baadhi ya mataifa yaliyoweka sera ya kuachana na magari yanayotumia petroli na dizeli, badala yake watajikita katika matumizi magari yanayotumia gesi.
Amesema uwepo wa sera inayoelekeza kuhamisha matumizi kutoka kwenye mafuta kwenda kwenye gesi unavutia sekta binafsi kukimbilia kufanya uwekezaji.
“Sekta ya gesi ni eneo linalopaswa kupewa kipaumbele kwani ina uwezo wa kubadili uchumi kwa kiwango kikubwa ndani ya muda mfupi,” amesema.
Amesema uchumi wa gesi ni mkubwa na unakwenda kubadilisha mfumo wa nishati hasa kupunguza gharama za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa na kupunguza utegemezi wa Dola ya Marekani.
“Matumizi ya gesi ni nafuu kuliko petroli na dizeli na matumizi yake yakiwa makubwa yatakwenda kushusha gharama za matumizi viwandani, usafirishaji wa watu na bidhaa, hivyo watu watakwenda kupata bidhaa kwa gharama nafuu,” amesema.
Dk Lawi amesema sababu ya gharama ya bidhaa kuwa kubwa ni kutokana na gharama za usafirishaji na uendeshaji kuwa kubwa, hivyo gesi ikipewa kipaumbele itakwenda kuonyesha mabadiliko kwenye uchumi.