
Na Mwandishi Wetu, Arusha.
MKUU wa Mkoa wa Arusha, Paul Christian Makonda, ameahidi kumjengea nyumba ya vyumba viwili Penina Petro (70) mkazi wa Kijiji cha Siwandete Kata ya Kiranyi Wilaya ya Arusha mkoani humo.
Makonda ametoa ahadi hiyo baada ya bibi huyo kuangua kilio na kudai ananyanyasika na familia yake kutokana na kutojaliwa kupata mtoto.
Amesema nyumba aliyokuwa anaishi awali imeanguka na kuomba msaada kwa familia yake ambapo wamegoma kumjengea kwa madai hana mtoto na anaweza kufa wakati wowote na hapatakuwa na mrithi wa nyumba hiyo.
Makonda baada ya kumsikiliza bibi huyo alimuomba aondoe uchungu aliokuwa nao na kuwasamehe wote waliomfanyia ukatili huo huku akimuahidi ifikapo Mei 13 mwaka huu atamjengea nyumba ya vyumba viwili na kumpatia ulinzi.