By Mary Shirima
Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi ametaja sababu mbili za kusogeza mbele shughuli ya uhakiki wa vyama hadi Julai 26 mwaka huu, ikiwemo kufanyia kazi hoja zilizojitokeza kwenye mkutano uliofanyika baina ya ofisi yake na viongozi wa vyama hivyo.
Sababu nyingine ni kutoa mafunzo kwa siku mbili kwa timu ya ofisi yake itakayohusika na kutekeleza shughuli hiyo kwa kuvizungukia vyama 19 ambayo vimepata usajili wa kudumu ili kuweka maboresho na kupata matokeo mazuri katika kazi hiyo.
Jaji Mutungi, juzi akiwa kwenye mkutano na viongozi wa vyama vya siasa nchini wa kuwapa elimu ya kuwaandaa kuelekea kwenye shughuli hiyo aliwatangazia kwamba Julai 20 mwaka huu kazi ya uhakiki ilipaswa kuanza.
Akizungumza na leo Julai 21,2023 Jaji Mutungi alitoa sababu hizo mbili huku akieleza ofisi yake ingefanya makosa kama wangeanza shughuli hiyo bila kuzingatia hoja walizozitoa katika mkutano huo.
“Katika kikao kile kuna baadhi ya viongozi walikuwa wanalalamika tunakuja kama mapolisi, tumeona tusipuuzie hoja zao na sisi tunajiweka katika mazingira kusudi wale wanaoenda kufanya uhakiki wakazingatie maelekezo,”amesema Jaji Mutungi.
Amesema kutokana na hoja zilizoibuliwa na umuhimu wa shughuli hiyo waliona bora wasogeze mbele badala ya kuanza Julai 20 sasa waanze rasmi Julai 26 Mwaka huu.
“Kuna mambo ambayo yamejitokeza na sisi lazima tuyazingatie vinginevyo na tutakuwa hatua haja ya kushare, kikao kilikuwa ni kuwaandaa kabla ya uhakiki sasa.
Na wenyewe wameibua hoja ambazo tunaona tujitoe kuipitisha timu ambayo itakuwa inazungukia katika shughuli ya uhakiki nayo ipewe mafunzo kwanza lengo na madhumuni tunataka kuboresha na kupata matokeo mazuri ya uhakiki,” amesema.
Baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa nchini wakiwa kwenye mkutano wa pamoja